Waziri wa Fedha, Saada Mkuya leo atawasilisha bajeti ya Serikali kwa mwaka wa fedha wa 2015/16 ambayo wachambuzi wameielezea kuwa itakuwa na unafuu kwa wananchi kutokana na Uchaguzi Mkuu utakaofanyika Oktoba, mwaka huu.
Wakati wachambuzi wakiielezea kuwa ni bajeti ya uchaguzi, wabunge waliozungumza na Mwananchi jana walisema hawatarajii kitu kipya kwa kuwa kila mara wamekuwa wakiipitisha kwa makofi, lakini utekelezaji unakuwa mdogo na sababu zimekuwa ni ukosefu wa fedha.
Bajeti hiyo ya Sh22.4 trilioni, ongezeko la asilimia 16 kulinganisha na bajeti ya mwaka 2014/15 ya Sh19.6 trilioni, inatarajiwa kuboreshwa kwenye maeneo kadhaa baada ya wabunge kuchachamaa wakati wa uwasilishaji wa bajeti za wizara mbalimbali.
Wabunge waligeuka mbogo wakati wa upitishaji wa bajeti za wizara hasa kutokana na Serikali kushindwa kupeleka fedha za miradi ya maendeleo kwa angalau asilimia 50 ya fedha zilizotengwa kwenye bajeti inayomalizika, na wakati mwingine ilibidi Waziri Mkuya asimame kutoa ahadi kuwa masuala hayo yangepelekwa kwenye Kamati ya Bajeti kuboreshwa.
Hii ni mara ya pili kwa Waziri Mkuya kuwasilisha bajeti baada ya kufanya hivyo kwa mara ya kwanza mwaka jana alipowasilisha ya mwaka unaomalizika Juni 30.
Akiwasilisha taarifa ya mwelekeo wa bajeti kwa mwaka wa fedha 2015/16 unaoanza Julai Mosi, Mkuya alisema Serikali imepania kupunguza utegemezi wa fedha kutoka kwa wahisani na wafadhili kutoka asilimia 14.8 hadi asilimia 8.4 na kwamba itajikita zaidi katika kukusanya kodi kwa kuhimiza matumizi ya vifaa vya kielektroniki.
Wachambuzi walihojiwa na Mwananchi jana walielezea bajeti hiyo kuwa italenga zaidi kutoa matumaini kwa wananchi, lakini itakuwa vigumu kutekelezeka.
“Kwa mfano, kupunguza utegemezi kwa wahisani ni tumaini zuri, lakini shaka ni malimbikizo ya madeni kwa makandarasi, walimu na taasisi nyingine zinazojiendesha. Tatizo jingine ni bajeti kidogo iliyotengwa kwa maendeleo,” alisema Profesa Humphrey Moshi kutoka Idara ya Uchumi ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM).
Naibu Katibu Mkuu wa Chama cha Walimu Tanzania (CWT), Ezekiah Oluoch alisema bajeti hiyo haina matumaini kwa watumishi wa umma hususani walimu nchini kutokana na mambo mengi kutoonekana.
“Niliangalia kwa umakini bajeti ya elimu na kuichambua, lakini mambo mengi ya msingi hayajaonekana. Mfano fungu la kulipa madeni ya walimu wastani wa Sh20 bilioni halipo, bajeti ya kuanzisha Tume ya Utumishi wa Walimu hakuna.”
Mbali na kupunguza utegemezi kwa nchi wahisani na wafadhili, Serikali pia ilitangaza nafuu kubwa katika ada na kodi mbalimbali za ardhi, baada ya kuzishusha kwa wastani wa asilimia 50, jambo linaloonekana kuwa la kuwapa matumaini wananchi wakati huu wa kuelekea Uchaguzi Mkuu.
Katika taarifa ya mwelekeo wa bajeti kwa mwaka wa fedha 2015/16 unaoanza Julai Mosi, Mkuya alitangaza vipaumbele vyake, ikiwamo kugharamia uchaguzi mkuu, kukamilisha miradi inayoendelea, kuweka msukumo maalumu kwenye miradi ya umeme vijijini, maji vijijini na kuimarisha rasilimali watu.
SOURCE:MWANANCHI
- Blogger Comment
- Facebook Comment
Subscribe to:
Post Comments
(
Atom
)

0 comments:
Post a Comment